image

image

Sunday, June 2, 2013

dharurah ya kuwa na elimu sahihi na amali njema



     Uwajibu wa kuwa na elimu na kuifanyia kazi
Allaamah   swaalih   bin  Fawzaan   al-Fawzaan
Kwa hakika hakuna budi kwa muislamu kutafuta elimu na kuitendea kazi kwa amali. Na ni mambo mawili yaendayo sambamba. Kama Alivyosema Allaah (Ta’ala):  yeye ndiye Aliyemtuma Mtume Wake kwa uwongofu na Dini ya Haki. (04:33)  “al-Hudaa” ni elimu yenye manufa. “ad-Diyn-ul-Haqq” ni amali njema. Amali haisihi bila ya elimu, bali inakuwa ni upotofu. Wala haifai elimu bila ya amali, bali inakuwa ni hoja dhidi ya mwenye nayo. Ikijumuika elimu na amali – elimu sahihi na amali njema kwa Muislamu anakuwa katika wale Aliyowaneemesha Allaah; katika Manabii, masaddiq, mashahidi na watu wema. Na mtu akichukua elimu [tu] akaacha amali, anakuwa katika wale walioghadhibikiwa [na Allaah]. Nao ni mayahudi na wanaojifananisha nao. Na mtu akifanya amali tu bila ya elimu, anakuwa katika waliopotea. Nao ni manaswara na wanaojifananisha nao katika wale wanaomuabudu Allaah kwa ujinga na upotofu. Na hili  lapatikana mwisho wa suraat-ul-Faatihah. Anasema Allaah(Ta’ala): Tuongoze katika  njia iliyonyooka. Njia ya wale Uliowaneemesha. (01:06-07)  Nao ni wale walioyajumuisha baina ya elimu yenye manufaa na amali njema. Si(ya wale)  walioghadhibikiwa. (01:07)  Nao ni wale waliochukua elimu wakaacha amali, hivyo wakaghadhibikiwa. Kwa kuwa wamemuasi Allaah kwa baswiyrah[ujuzi]. Wala waliopotea. (01:07)  Nao ni wale waliochukua(fanya) amali bila ya elimu. Huu ni upotofu na kupinda. Na amali hii haimfai mwenye nayo, bali inakuwa anajitaabisha na ataulizwa siku ya Qiyaamah. Hivyo ni lazima [mtu] kuwa na elimu yenye manufaa na amali njema. Na elimu lazima itangulie kabla ya [mtu kufanya] amali. Ni lazima kwa mtu kusoma vipi atamuabudu Allaah? Vipi atampwekesha Allaah(‘Azza wa Jalla)?  Vipi ataswali? Vipi atatoa zakaah? Vipi atafunga? Vipi atahiji na kufanya ‘Umrah? Lazima ajifunze kisha ndio alete amali zikifanywa kwa elimu, mpaka ziwe zimejengeka juu ya msingi sahihi. Akimtakasia Allaah(‘Azza wa Jalla)  Anasema Allaah(Ta’ala): basi jua ya kwamba hapana mungu ila Allaah, na omba maghufira kwa dhambi zako na za Waumini wanaume na Waumini wanawake. (47:19)
 Kaanza kwa elimu kabla ya kauli na amali. Na kaweka imam bukhaariy(Allaah amrehemu) mlango maalumu kutokana na Aayah hii akauita:
“Mlango unaozungumzia elimu kabla ya kauli na amali” Amechukua katika Aayah hii.   Ni lazima kwa Muislamu asome mambo ambayo yatamuwezesha kusimama na dini yake; Tawhiyd, ‘Aqiydah, swalah, Zakaah, Swawm, Hajj na ‘Umrah. Ni lazima kwa kila Muislamu. Haya ni fardhi ’ayn[1]  kwa kila muislamu, sawa wanaume na wanawake, mwarabu na asiyekuwa mwarabu. Ni lazima kuyajua.  Hapewi udhuru yeyote kwa kutoyajua haya.  Na haya ni sahali[kujifunza nayo] – himidi zote ni Zake Allaah. Maulamaa wamefanya risalah za mukhtasari zilizowazi. Mtu anaweza kujifunza nayo kwa nusu saa au dakika kama kumi akastafidi, vipi  atamuabudu Mola wake(‘azza wa jalla). Hali kadhalika asome elimu kwa wanachuoni, asome  elimu kwa wanachuoni. Asitosheke na kusoma [vitabu na mikanda tu], bali asome kwa wanachuoni ima madrasah au sehemu za majlisi za dhikr kwa Mashaykh wanaofunza katika misikiti. Hali kadhalika asikilize mihadhara, wito wa kielimu, khutbah ya ijumaa, barnamiji zinazorushwa kwenye vyombo vya habari katika idhaa ya Qur-aan Tukufu –kuna barnamiji za kielimu zenye kunufaisha. Anufaike nazo mtu. Baada ya kusomwa Qur-aan kunakuja barnamiji za kielimu. Elimu inakukuta kila mahala na wewe uko kwenye kitanda chako, kwenye gari yako nakadhalika; unafungua idhaa unasikiliiza. Hii ni heri nyingi. Hali kadhalika katika mambo utayostafidi kwayo ni kuuliza wanachuoni. Anasema Allaah(Ta’ala); basi waulizeni wenye ukumbusho kama nyinyi hamjui. (16:43)   Unapotatizika na jambo, uliza wanachuoni wakubainishie kinachokutatiza. Njia nyingi ni sahali –himidi zote ni zake Allaah.  Kasema Mtume (swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam): “Mwenye kuchukua njia anatafuta humo elimu, Allaah Humsahilishia kwayo njia ya kwenda peponi.”  Vikao vya dhikr katika misikiti au madrasah, zote hizo ni khair- himidi zote ni zake Allaah. Lakini tatizo ni kwa Yule asiyetaka kusoma na akabaki katika ujinga wake. Hasomi wala hastafidi. Na huenda akafanya ‘ibaadah kwa mfumo usiyo sahihi ilihali naye hajui. Hii ndio natija ya kutosoma na kustafidi. Yeye ndiye kaipotoa nafasi yake na kapoteza wakati wake. La sivyo elimu ni sahali  - himidi zote ni zake Allaah. Si lazima uwe  mwanachuoni kigogo. Yatosheleza ukajifunza mambo ya dini yako, na zaidi ya hapo ni khayr; Katika mambo ya mu’amalat, mirathi,auqaf,wasia na mambo mengine wanayoyahitajia watu. Haya ukiweza jifunze nayo ustafidi na unufaishe pia wengine hii ni khayr.  lakini aina ya kwanza mambo ya ‘ibaadah [fardhu ‘ayn] haya hapewi udhuru yeyote kwa kutoyajua. Ninamuomba Allaah Atuwafikishe sote kwa kauli njema na amali.
Muhadhara huu unapatikana kwa njia ya sauti katika link hii hapa chini http://www.youtube.com/watch?v=XHrFlsa2D0s
Swalah na salaam zimuendee Mtume wetu Muhammad(swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam)  na ahli zake na maswahaba zake na atakayemfuata kwa wema